1 Yohana 4 – Kutoka kupotea hadi kumpenda jirani yako

Mwandishi: 
Erkki Koskenniemi
Mtafsiri: 
Richard Ondicho

Soma au sikiliza Waraka wa Kwanza wa Yohana mtandaoni (Neno Bibilia Takatifu SNT, Bible Gateway)


Tumeendelea hadi sura ya nne ya waraka wa kwanza wa Yohana. Sura hii ni sehemu ya kipande kipana zaidi (sura ya 4-5), ambapo mada ni mafundisho sahihi yanayoongoza kwa maisha sahihi. Katika sura ya nne, kwanza kuna onyo dhidi ya mafundisho ya uongo na kisha mazungumzo kuhusu kumpenda jirani yako.

4:1-3: Usimwamini kila mhubiri!

Wakati waraka huu ulipoandikwa, kulikuwa na mafundisho mengi magumu ya uongo yaliyokuwa yakifanya kazi. Ndiyo maana kulikuwa na sababu nzuri ya kuwaonya watu wa Mungu kwamba kila mhubiri si lazima awe katika kazi ya Mungu. Wasikilizaji wanapewa kipimo cha kupambanua kati ya roho sahihi na roho potofu. Yeyote ambaye hakiri kwamba Yesu ni Kristo na amekuja katika mwili ni roho ya uongo, na anayekiri hivyo, ni wa Mungu.

Kwa kawaida ni vigumu sana kuwatambua walimu wa uongo ambao waandishi wa Agano Jipya wanawakosoa, kwa sababu tunachoweza kujua kuwahusu ni maonyo tunayoyasoma tu. Katika hali hii, fundisho la uongo, ambalo lilikuwa likiiathiri kanisa la awali na ambalo halikukubalika, linajulikana vizuri. Kulikuwa na wale waliofundisha kwamba Yesu alikuwa kiumbe cha kiroho, si binadamu wa kweli. Walidai kwamba kwa kuwa hakuwa binadamu wa kweli, hakuteseka pia, wala hakufa kwa vyovyote. Na kwa kuwa hakufa, wala hakulipa bei kwa dhambi zetu wala hakutekeleza Upatanisho. Walifundisha kwamba Yesu alikuwa kama mwanga wa ghafla uliowaonyesha watu wote njia sahihi ya nuru. Fundisho hili lilikuwa magugu, na kanisa la awali lilikuwa na kazi nyingi ya kuling'oa.

Tunapotumia aya hizi katika wakati wetu wenyewe, kwanza tunaona kwamba si vibaya wala si kuchukiza kuendelea kuwachunguza wahubiri. Badala yake, neno la Mungu linatutia moyo waziwazi kufanya hivyo. Fundisho la uongo ni kitu hatari na linakiuka utakatifu wa Mungu. Hatupaswi kukubali kulisikiliza.

Pili, tunagundua kwamba ulimwengu haukubadilika hata kidogo: fundisho lile lile la uongo linafanya kazi hata sasa miongoni mwetu. Katika siku zetu, ni Anthroposofia ya Rudolf Steiner (au, inayohusiana nayo kwa karibu, theosofia au christosophia). Mafundisho hayo hayo yanaunda msingi wa uzushi huu. Hii ndiyo inayofanya shule za Steiner kuwa na utata kutoka mtazamo wa Kikristo.

Uzushi unashindwa kwa kuukataa 4:4-6

Wapokezi wa waraka hawakuyakaribisha mafundisho ya uongo bali waliyakataa. Kwa hivyo walikuwa wameshinda jaribu la fundisho la uongo. Haikuwa hekima yao wenyewe iliyowahifadhi salama bali upendo wa Mungu. Mungu alikuwa amelinda watu wake. Na ingawa mafundisho yaliyosukumwa na walimu wa uzushi yaliendana vizuri sana na mawazo ya watu – bila shaka mafundisho yanayoongozwa na matakwa ya ulimwengu yanaendana na ulimwengu – bado kulikuwa na kundi la watoto wa Mungu ambao walikuwa salama dhidi ya kujikwaa. Neno la kitume ni neno la Mungu: wale ambao Mungu anawagundulia, wanawasikia mitume. Wale wanaomkana Mungu, wanakana pia neno la kitume. Mpaka ni wazi na rahisi kiasi hicho.

Tena, tunajifunza mambo mengi kuhusu uzushi. Watu wanaweza kupenda uzushi, tofauti na neno la Mungu. Mhubiri wa uongo anaweza kuheshimiwa sana miongoni mwetu, kwa sababu mafundisho sahihi mara nyingi yanaudhi sana asili yetu ya dhambi. Ingekuwa rahisi zaidi kujisalimisha na kuacha mafundisho ya Biblia – lakini hapo Mungu mwenyewe angetupiliwa mbali! Kinachokuwa hatarini ni halisi sana: yeyote anayekataa neno la kitume anamkataa Mungu pia na yuko katika nguvu ya roho ya udanganyifu.

Pendaneni! 4:7-12

Mtume anarudi tena kwenye mada ya maisha sahihi ya Kikristo yanayotokana na mafundisho sahihi na imani. Aya za 7-12, hasa, ni kama wimbo, mazungumzo mazuri sana kuhusu upendo wa Mungu na kuhusu upendo wa mtu wa Kikristo. Neno 'upendo' linajitokeza tena na tena. Hapa tunayo, kwa namna fulani, mwenzake wa "Wimbo wa Upendo" maarufu ulioandikwa na mtume Paulo (1 Wakorintho 13).

Tunapaswa kuona mpangilio sahihi katika sehemu hii: kuna mazungumzo yenye msisitizo mkubwa kuhusu upendo wa Kristo na baada ya hapo, hitimisho zinatolewa kutoka kwake. Tunapozungumza kuhusu upendo, kwa kweli, kuna sababu nzuri ya kwanza kuonyesha upendo wa kweli, thabiti, na wenye bidii. Unaonekana kwa kila mtu katika msalaba wa Kristo katika Mlima Golgotha. Mungu alimtoa Mwanaye wa pekee ulimwenguni. Damu yake ilileta Upatanisho kwa dhambi zetu. Uhusiano wetu na Mungu umesahihishwa, kwa sababu Mungu aliusahihisha. Upendo wa kweli hauko katika mioyo yetu bali katika moyo wa Mungu Baba. Mioyo yetu inapata joto lakini inapoa tena. Neema ya Mungu haibadiliki. Yeyote anayeelewa hili amepata msingi imara ambao utasimama katika dhoruba zote.

Ni kwa Mkristo kutoa hitimisho kutoka kwa upendo wa Mungu. Kwa sababu Mungu alitupenda, ni kwa ajili yetu kumpenda jirani yetu. Kwa namna hii, wema wa Mungu unapewa nafasi katika maisha yetu. Mto wa baraka utatiririka kupitia Wakristo katika ulimwengu huu baridi na mwovu. Badala ya chuki kutakuwa na msamaha, badala ya kutisha na kulipiza kisasi kutakuwa na baraka. Kwa namna hii, Ufalme wa Mungu utachukua sura hata katika ulimwengu huu, ingawa kwa sehemu tu, lakini hata hivyo, malimbuko yaliyoletwa na upendo wa Mungu yanakusanywa hata katika wakati huu wa sasa, na tunamshukuru Baba Mungu wetu mwema kwa hayo.

Kana kwamba kwa kupita tu, Yohana anasema maneno ambayo yamewashangaza wasomaji wengi wa Biblia. Kwa nini Yohana anasema kwamba hakuna mtu aliyemwona Mungu? Vipi kuhusu Ibrahimu? Au Musa? Au Isaya? Au Ezekieli? Kuna historia ndefu ya imani ya Kiyahudi nyuma yake. Mataifa ya wapagani walitengeneza sanamu za miungu na kuziabudu. Kwa watu wa Mungu katika Agano la Kale ilikuwa ukweli kamili kwamba hakuna binadamu anayeweza au anaruhusiwa kutengeneza sanamu ya Mungu. Yeye hayupo katika umbo la binadamu kwa namna ambayo fundi wa miungu anafikiri. Bwana ni kitu kingine kabisa. Kwa sababu hii, mafundisho ya baadaye ya Kiyahudi kuhusu suala hili ni ya tahadhari sana na hayakutaka kutoa nafasi yoyote ya kueleweka vibaya kwa Agano la Kale kwa njia yoyote. Ndiyo maana ilielezwa kwamba watakatifu katika Agano la Kale hawakumwona Mungu kwa kweli bali utukufu wa Mungu tu. Tunaweza kuelewa hili kwa kutazama jua; kwa kweli hatuoni jua lenyewe bali mwangaza wake wa kupofusha.

4:13-21 Upendo na uhakika wa wokovu

Tunawezaje kudumu katika imani hadi mwisho? Jibu la Yohana ni kwamba jambo hili ni kazi ya Roho Mtakatifu wa Mungu. Wale wanaostahimili hadi mwisho ni wale wanaomwamini Mwana wa Mungu. Mungu atawahifadhi hadi siku ya hukumu. Tunapaswa kuishi tukimpenda jirani yetu, kwa sababu ni kwa namna hii Mungu atafanya kazi kupitia kwetu. Uhakika wa imara kwa Mungu unafukuza hofu na kutupa amani. Yeyote anayeogopa uharibifu wa milele na ghadhabu ya Mungu bado hajakamilishwa katika upendo na bado hajajifunza kikamilifu kujua kina cha upendo wa Mungu. Kwa upande mwingine, wale wanaokataa kumpenda jirani yao bila shaka wanamkataa Mungu wakati huo huo.

Tena, tunajifunza mambo mengi kutoka sehemu hii fupi. 'Upendo' katika nyaraka za Yohana haumaanishi hisia bali kitendo. Hakuna mtu anayeweza kusema anampenda jirani yake na wakati huo huo kumwacha jirani akifa njaa. Wala hawawezi kusema kwamba wanampenda Mungu na bado kuendelea kuishi kwa makusudi kinyume na neno la Mungu. Imani, mafundisho sahihi, na upendo vyote vinashikamana. Hawezi kuwepo mmoja bila wengine, wala wengine bila mmoja. Ikiwa tunaweka mafundisho na maisha dhidi ya kila moja, jambo ambalo mara nyingi hufanywa, tuko katika njia potofu kabisa. Hivi viwili vinashikamana bila shaka na bila kutengana.

Zaidi ya hayo, tunaweza kuona uhakika wa wokovu ni nini. Ni kujua upendo wa Kristo, na ni imani thabiti katika neema ya Mungu. Uhakika huu haupatikani ndani yetu wenyewe, wala katika imani yetu. Uko ndani ya Kristo na upendo wake. Mwenye dhambi anapokuwa na imani kwa Bwana wa msalaba, miali ya moto wa jehanamu inazimwa, na amani ya Mungu itatupa tayari ladha ya awali ya furaha ya mbinguni. Hatuwezi kuiamini au kuielewa vizuri, na sababu ya hili ni kwamba sisi ni wapole wa moyo kuamini neno la Biblia. Inaonekana haiwezekani kwamba mimi, kama nilivyo, ninaweza kuwa mtoto wa Mungu. Lakini ni kweli, kwa sababu hii ndiyo hasa Biblia inayotufundisha!