Waraka wa Pili wa Yohana – Mwongozo wa Masomo

Mwandishi: 
Erkki Koskenniemi
Mtafsiri: 
Richard Ondicho

Soma au sikiliza Waraka wa Pili wa Yohana mtandaoni (Neno Bibilia Takatifu SNT, Bible Gateway)


Masomo makubwa kutoka katika nyaraka mbili fupi

Nyaraka fupi zaidi katika Agano Jipya mara nyingi zinapuuzwa bila sababu ya kutosha. Mambo mengi yanaelezwa kwa ufupi na kwa uwazi ndani yake. Sasa tutasoma nyaraka mbili za Yohana mfululizo. Waraka wa Pili wa Yohana na Waraka wa Tatu wa Yohana zote zinachukua ukurasa mmoja tu katika Biblia zetu. Hata hivyo, zina masomo ambayo ni vyema tuyatafakari.

Haijulikani kwa uhakika nyaraka hizi mbili ziliandikwa lini hasa (karibu mwaka 100). Wala hatujui kwa uhakika mwandishi wake. Hata hivyo, mwandishi huyu kwa wazi ni yule yule aliyeandika Waraka wa Kwanza wa Yohana. Nyaraka zote mbili, 2 Yohana na 3 Yohana, zinashughulikia kanisa na mafundisho ya uongo, lakini kutoka pande tofauti kabisa. Ni vigumu kubainisha ni ipi iliyoandikwa kwanza, na vilevile uhusiano wake na Injili ya Yohana.

Barua kwa bibi mteule – bibi mteule ni nani? 2 Yohana 1-3

Waraka wa Pili wa Yohana unaelekezwa kwa 'bibi mteule'. Usemi huu na 'dada mteule' katika mstari wa 13 vinamaanisha kanisa la mahali fulani. 'Watoto' wa 'dada mteule' ni wanachama wa kanisa hilo, yaani Wakristo.

Nyuma ya usemi 'bibi mteule', kuna picha nyingi za Biblia ambazo zinastahili kuchunguzwa. Katika Agano la Kale, Yerusalemu mara nyingi inaitwa 'binti Sayuni', na uhusiano kati ya Mungu na Israeli mara nyingi unalinganishwa na uhusiano kati ya mume na mke. Kwa sababu ya taifa teule, uhusiano huu mara nyingi si wa furaha, na manabii wanawashutumu watu kwa 'uzinzi'. Hivyo, Mungu ni mume mwenye upendo na watu ni kama mke asiye mwaminifu ambaye hajali mpenzi wake bali anaabudu sanamu. Mbali na Kitabu cha Hosea, picha hii inapatikana katika Yeremia (Yeremia 3) na katika Ezekieli (Ezekieli 16 na 23). Kwa upande mwingine, kuna uhusiano mzuri wenye upendo katika Kitabu cha Wimbo Ulio Bora: ingawa mashairi haya kwa asili yanahusu uhusiano kati ya mwanamke na mwanaume, tangu zamani yamefasiriwa kuwa yanazungumzia uhusiano kati ya Mungu na Israeli.

Katika Agano Jipya, picha hiyo inachanua upya. Mifano ya Yesu mara nyingi inatupeleka kwenye karamu ya arusi ya Mashariki ya Kati. Yohana Mbatizaji anafurahi kwamba aliweza kutenda kama msemaji, rafiki ya bwana arusi, kati ya Kristo na mpenzi wake (Yohana 3:22-36). Paulo anasema kwamba aliwaposa Wakristo kwa Kristo kama bikira safi (2 Wakorintho 11:2), na anatumia picha ya Kristo na bibi arusi wake pia katika Waefeso (Waefeso 5:21-23). Kitabu cha Ufunuo, katika sura ya 12, kinalinganisha kanisa na mwanamke mwenye watoto (=Wakristo), lakini katika sura za mwisho kinafungua milango ya mbinguni na kutuchora picha ya ajabu ya arusi ya Mwana-Kondoo.

Maneno kuhusu bibi mteule, yaani kanisa la mahali fulani, na dada zake, yaani kanisa lingine la mahali fulani, sasa yanahusishwa na picha hii tajiri. Kama vile Mungu ni Baba yetu, kanisa ni mama yetu. Wakati huu, picha hii nzuri inaenezwa pia hadi kanisa la mahali fulani. Mkristo kamwe hawi peke yake bali daima ni sehemu ya familia ya Mungu. Tangu zamani imesemwa kwamba huwezi kumweka Mungu kuwa Baba yako ikiwa huna kanisa kuwa mama yako. Waraka huu mdogo unasisitiza umuhimu wa kanisa la mahali fulani na, wakati huo huo, unalitakia wajibu.

Tupendane sisi kwa sisi 2 Yohana 4-6

Kama ilivyo mara kwa mara katika Waraka wa Kwanza wa Yohana, mwandishi anasisitiza kumpenda jirani. Upendo sasa unazungumzwa kwa undani zaidi: Upendo si kitendo chochote tu, hata kama kinaweza kuitwa hivyo. "Na huu ndio upendo, kwamba tuenende sawasawa na amri zake." Kwa hivyo, mwandishi kwa sababu fulani anafafanua zaidi upendo ni nini. Hatujui sababu halisi, lakini katika wakati wetu, maneno haya yanagusa sana. Katika nchi yetu, upendo mara nyingi unapingana na amri za Biblia. Upendo unapodai, Biblia lazima ipishe. Mtazamo huu hauendani na Waraka wa Pili wa Yohana. Labda tunapaswa kunukuu kauli kali hii, "Mungu ni upendo, lakini upendo si Mungu." Ikiwa uelewa wetu wa upendo unapotoka kutoka katika maelekezo ya Biblia, si Biblia iliyo na kosa bali ni uelewa wetu.

Wafungieni milango walimu wa uongo! 2 Yohana 7-11

Walimu wa uongo ndio sababu ya kutumwa kwa waraka huu. Walitembea kutoka kanisa hadi kanisa na kueneza ujumbe uliokuwa kinyume na imani ya kimitume. Hatujui hasa walifundisha nini. Inatosha kwetu kwamba hawakukiri kwamba Yesu alizaliwa kuwa Kristo ulimwenguni. Kwa wazi, walimu hawa walikana kwamba Yesu alizaliwa kuwa mwanadamu wa kweli na kwamba alisulubiwa na kufufuka kutoka kwa wafu.

Maelekezo yaliyopewa kanisa ni wazi kabisa. Hakuna mtu anayepaswa kumkaribisha mhubiri wa uongo. Kutaniko lote lazima liwakatae. Wale wanaofungua nyumba zao kwa walimu kama hao wanashiriki katika dhambi zao. Uzushi wao ni hatari. Kwa hivyo lazima uzuiwe kabisa kanisani. Maelekezo haya yanaeleweka yanapotazamwa kutoka mtazamo wa kimatendo sana.

Wakristo wa kwanza walijua vyema kwamba kuanzisha kanisa jipya mjini kulikuwa kazi ngumu kwa mgeni. Ilikuwa rahisi zaidi ikiwa mhubiri mtembezi angeweza kupata hata nyumba moja ambayo ingemfungulia mlango. Mwalimu wa uongo sasa alipaswa kuzuiwa asipate hata nyumba hiyo moja, bali alipaswa kuanza juhudi zake sokoni na peke yake.

Waraka huu mdogo unatupa mengi ya kutafakari. Katika kanisa letu, kuna mielekeo inayoenda pande nyingi. Kwa upande mmoja, wachungaji katika makanisa yetu wanaweza kufundisha karibu chochote na hata kupotoka kutoka mafundisho ya Biblia bila hofu ya kupoteza kazi zao. Kwa upande mwingine, walimu waliojitolea kwa neno lililoandikwa la Biblia wakati mwingine wamekuwa katika hali ngumu sana. Suluhisho linalotolewa mara kwa mara ili kuliweka kanisa katika umoja ni kanuni ya zamani kwamba lazima tuache maua elfu yachanue. Inaweza kuwa suluhisho la muda, lakini wakati huo huo, lazima kusisitizwa kwamba hilo si jambo ambalo Biblia inatushauri kufanya. Badala yake, Waraka wa Pili wa Yohana unazingatia maneno ya Yesu, "Kila mmea ambao Baba yangu wa mbinguni hakuupanda, utang'olewa." (Mathayo 15:13).

Salamu za mwisho 2 Yohana 12-13

Mwandishi anamalizia barua yake kwa salamu fupi na kutoa hamu yake ya kuja hivi karibuni na kujiunga nao kanisani na kuwa katika mawasiliano ya moja kwa moja na 'bibi mteule'. Katika waraka huu, anayezungumza ni mtu mwenye mamlaka yasiyopingika ambaye 'dada' kadhaa wa bibi mteule lazima walikuwa wakimsikiliza. 'Mzee' hahitaji kujitambulisha. Mamlaka ya kitume yanajisemea yenyewe.